TAFITI: Instagram ndiyo mtandao hatari zaidi kiafya

Mtandao wa Instagram umeorodheshwa kuwa mtandao wa kijamii ambao una madhara zaidi kwa afya ya kiakili ya vijana.

Katika tafiti zilizofanywa nchini Uingereza, vijana 1,479 wa miaka kati ya 14 na 24 waliombwa kueleza utathmini wao kuhusu mitandao mbalimbali ya kijamii kwa kuzingatia wasiwasi, mfadhaiko, upweke, dhuluma na sifa za kimwili.

Mtandao wa Instagram ndiyo uliongoza kwa kuwa na madhara zaidi kwa vijana ukilinganisha na mitandao mingine ya kijamii

Mashirika ya hisani kuhusu afya ya kiakili yametoa wito kwa makampuni kuimarisha usalama wa watu wanaotumia mitandao ya kijamii.

Utafiti huo uliofanywa na taasisi ya Royal Society for Public Health unasema mitandao ya kijamii inafaa kutambua watu wanaotumia mitandao ya kijamii kwa kupitiliza na pia wale wenye matatizo ya kiakili.

Inakadiriwa kuwa 90% ya vijana hutumia mitandao ya kijamii, na hivyo ndio huathirika zaidi.

Utafiti huo uliwauliza washiriki maswali kuhusu iwapo YouTube, Instagram, Snapchat, Facebook na Twitter zina madhara kuhusu afya yao na hali yao.

Washiriki walitakiwa waipe alama mitandao ya kijamii kuhusu masuala 14 ya afya na hali yao.

Kwa kufuata vipimo vyao, YouTube ilichukuliwa kuwa yenye manufaa mengi zaidi katika afya ya kiakili, ikifuatwa na Twitter na kisha Facebook.

Snapchat na Instagram zilikuwa na alama za chini kabisa kwa jumla.

Shirley Cramer, afisa mkuu mtendaji wa RSPH, alisema: “Inashangaza kuona Instagram na Snapchat zikiorodheshwa kuwa na madhara zaidi kwa afya ya kiakili na hali nzuri ya vijana – majukwaa haya mawili sana huangazia sura na sifa nzuri na mtu. Mitandao hii miwili inaonekana kuwafanya vijana wengi wajihisi kwamba hawatoshi au wana mapungufu fulani na hivyo kuwaongezea wasiwasi.“.

By Godfrey Mgallah

Related Posts

Post a Comment